No copying

Thursday, 3 August 2017

MAMBO MANNE YAKUPASAYO KUFANYA/KUTENDA KATIKA WOKOVU WAKO.


UTANGULIZI:
Bwana YESU asifiwe sana wana wa  MUNGU. Leo nina ujumbe ambao unamuhusu kila mtu aliyeamua kuokoka na mwenye safari ya kwenda mbinguni. Yapo mambo mengi sana ambayo kila mwamini anatakiwa kufanya na kuyafuata yaani kuyaishi  katika wokovu wake. 



Tuangalie kwanza maana ya “WOKOVU”
WOKOVU…Ni mpango wa MUNGU wa kumtoa mwanadamu kutoka katika himaya ya shetani (chini ya nguvu za giza) na kumuingiza katika himaya ya MUNGU kwa njia ya YESU KRISTO. (Wakolosai 1:13, Luka 1:78-79; Isaya 9:2)

Yesu Kristo alikuja kutuokoa (Yohana 3:16) na wale wote waliomwamini wameokolewa yaani wameokoka. (WARUMI 10:9).
Katika mtazamo wangu nimeona yapo mambo manne ambayo ni ya lazima sana kwa kila mwamini. Mambo haya ni kama yafuatayo:-

1 KUSOMA NENO, KULITAFAKARI NA KULIISHI.
Hapa namaanisha kusoma Biblia. Biblia ni nini?
Biblia ni mkusanyiko wa vitabu ambavyo viliandikwa na watu wakiongozwa na Roho Mtakatifu. Katika kipengele hiki tutaangalia zaidi umuhimu wa kusoma neno la MUNGU au Biblia. Kwanza kabisa naomba tutambue kuwa BIBLIA ni neno au sauti ya MUNGU.
Kila mwamini lazima awe na ratiba yake ya kusoma neno la MUNGU katika maisha yake ya kila siku. Watu wengi husoma Biblia hasa siku za ibada yaani Jumapili au siku ambazo hukusanyika kwa ajili ya ibada. Sasa tuangalie baadhi ya umuhimu wa kusoma neno la MUNGU (BIBLIA)

A NI MWONGOZO WA MAISHA YA KILA SIKU.
Katika maisha yetu ya kila siku hasa wale tunaomwamini YESU kama mwokozi wetu, Biblia ndiyo mwongozo wa maisha yetu. Kama ilivyo nchi kwmba ina mwongozo wake ambao ni katika, kumbe hata sisi tunaweza kusema kuwa katiba yetu ya KIROHO ni BIBLIA. Kwa kusoma Biblia ndipo utakapojua njia za kuendea au njia zipi usienende nazo ili usije ukamkosea  MUNGU wako.
ZABURI 119:11 Moyoni mwangu nimeliweka neno lako, Nisije nikakutenda dhambi.
Daudi alijua kabisa kwamba bila kuliweka neno la MUNGU moyoni mwake basi katika kuishi kwake angekuwa anamkosea MUNGU. Kwa hiyo ili uweze kuishi bila kukosea ni lazima uhakikishe unaliweka neno la MUNGU ndani yako.
ZABURI 119:105 Neno lako ni taa ya miguu yangu, Na mwanga wa njia yangu.
Neno la MUNGU Daudi kalifananisha kama taa ya miguu yake. Kazi ya taa ni kumulika gizani ili kutoa Nuru uweze kuona hata kama kuna shimo huwezi kutumbukia. Kwa hiyo Biblia pia inatupa mwanga  ili wa jinsi gani uweze kuenenda katika maisha yako ya kila siku.
2Timothy 3:16 Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki
B.     NI CHAKULA CHA ROHO.
Binadamu ana ROHO na MWILI. Ili mwili uweze kuishi lazima mtu ale chakula na ndiyo maana tunakula chakula kila siku hadi milo mitatu. Kama mwili unalishwa vivyo hivyo hata roho inatakiwa ile ili iweze kukua. Sasa chakula cha ROHO ni NENO la MUNGU yaani Biblia. Mtu ambaye hasomi neno la MUNGU hawezi kukua kiroho. Kukua kiroho ni ile hali ya kuongezeka katika kuyajua mambo ya MUNGU na kulitendea kazi.  
1Peter 2:2 Kama watoto wachanga waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate kuukulia wokovu;
Baada ya kuokoka na kubatizwa kwa Roho Mtakatifu unakuwa umezaliwa mara ya pili. Chochote kinachozaliwa lazima kipate chakula ili kiweze kukua. Sasa kuna watu walizaliwa mara ya pili lakini wakakosa chakula matokeo yake wameugua kwashakoo ya kiroho/wamedumaa na siku zote wamebaki kuwa kama watoto. Hii inasababishwa na wao kutokula chakula ambacho ni neno la MUNGU.

C.     NI SILAHA DHIDI YA ADUI
Silaha ni kifaa au kitu kinachotumika katika  kujilinda na maadui. Wapo maadui wa aina mbili kama vile tulivyoona hapo juu kuwa kuna mwili na roho; kuna maadui wa mwili na maadui w kiroho. Maadui wa kimwili unapamba nao kwa silaha za mwili. Pia maadui wa kiroho unaambana nao kiroho. Hapa nitazungumzia kwa habari ya silaha za kiroho tu maana neno la MUNGU linasema katika Warumi 8:14 Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndiyo wana wa Mungu. Kama mtu akiongozwa na roho ina maana hata katika kuenenda ni kiroho. Kwa hiyo vita yetu haipo katika mwili wa damu na nyama, bali katika ulimwengu wa  roho kama Waefeso  6:12 Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.
WAEFESO 6:13-17
Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.
Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani,
  na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani;
zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu.
Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu.
Ukiangalia mstari wa 17 unasema neno la MUNGU ni upanga wa Roho. Kazi ya upanga ni kukata vitu. Kwa hiyo kama ni upanga wa Roho basi yale mambo ambayo yanaletwa na adui shetani yanakatwa na neno la MUNGU.

Waebrania 4:12 Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.

2  MAOMBI.
Maombi ni mazungumzo  kati ya mwanadamu na MUNGU. Tunawasiliana na MUNGU kwa njia ya maombi. Kila aliyemwamini YESU kama Bwana na mwokozi wa maisha yake, automatically ni kwamba anamwamini MUNGU wa mbinguni aliyeziumba mbingu na nchi. YOHANA 15:23 Yeye anichukiaye mimi humchukia na Baba yangu. Mungu anapenda sana ushirika wa Karibu na watu  wake anapenda awe anasemezana nasi kila iitwapo leo na kumshirikisha katika kila jambo ndiyo maana anasema katika WAFILIPI 4:6 Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu.
Yani kila shida ulinayonayo MUNGU anataka aijue aweze kukusaidia. MUNGU yeye ni Baba yetu ndiyo maana anataka atusaidie mahitaji yetu. Mtoto siku zote husaidiwa na Baba yake. Kwa njia ya maombi ndipo unapoweza kumweleza MUNGU shida zako wala siyo njia nyingine.
MITHALI 3:5 Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe;
Angalia hapa YESU anavyosisitiza YOHANA 16:24 Hata sasa hamkuomba neno kwa jina langu; ombeni, nanyi mtapata; furaha yenu iwe timilifu. Hapa alikuwa anawambia wanafunzi wake waombe.
Maombi ni ya msingi sana mwana wa MUNGU. Yapo mambo ambayo hayawezi kufanyika kwako bila kuwa mwombaji. Hili tunaliona pia wakati wanafunzi wa YESU wameshindwa kutoa pepo akawambia katika MATHAYO 17:21 Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.

3 UTAKATIFU.
Utakatifu ni kuishi maisha ya kumpendeza MUNGU. Ni maisha ambayo  mtu  anaishi kwa kufuata taratibu zote za ki-MUNGU huku akiongozwa na neno La MUNGU yaani Biblia. Mtu yeyote anayetembea katika utakatifu aba sifa zifuatazo:-
a)      Ni mcha MUNGU.
b)      Anatii NENO la MUNGU, watumishi pamoja raia wengine.
c)      Ni mnyenyekevu wa Roho.
d)     Yuko tayari kukosolewa.
e)      Siyo mtu wa hasira.
f)       Ni mtu mwenye furaha na ana upendo kwa watu wote.
g)      Huitafakari sheria ya MUNGU wakati wote.

4 KUWALETA WENGINE KWA YESU.
Hapa nazungumzia kuhubiri habari njema za mwokozi YESU kwa mataifa yote. MUNGU anapenda sana sisi tufanye kazi ya kumnyang’anya shetani watu kwa njia mbali mbali. Na hili ni agizo alilitoa YESU mwenyewe katika MATHAYO 28: 19 Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu;
 20 na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.
Waamini wengi wamekuwa hawatii agizo hili. Hii inatokea kwa sababu wanafikiri kazi ya kuhubiri habari njema ni ya Wainjilisti tu au wachungaji. Tukisoma hayo maandiko hayakusema watu flani bali waliambiwa wote. Kila mtu aliyeokoka ni Mtumishi wa MUNGU na ana jukumu la kuhakikisha anaongeza wafuasi wa YESU kwa kuwahubiri kwa matendo yake pamoja  na kuwafuata mataifa na kuwambia habari njema za YESU KRISTO. MUNGU yeye alitupenda sana hata akamtoa YESU afe kwa ajili yetu. Na sisi inatakiwa tuwe na upendo kwa ndugu, jamaa na rafiki zetu kwa kuwambia furaha na uzima uliopo watakapomwamini YESU. Tusiwaachie tu wachungaji jukumu hili bali kila mmoja awajibike kwa jinsi MUNGU atakavyomuwezesha. Kama huwezi kuhubiri basi shiriki katika kazi hii hata kwa kutoa mali zako.
YESU anasema katika MATHAYO  12:30 Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya.
YESU alikuja ili kuwaokoa watu kutoka katika dhambi, shida, adha, mateso na vifungo mbali mbali. Sasa kama mtu wa MUNGU hushiriki katika kuyatenda hayo ina maana unatapanya. Maana kwa sasa watenda kazi ni sisi yeye alindoka akatuachia agizo ya kuiendeleza kazi hii.
Bwana YESU anasema katika  Luke 10:2 Akawaambia, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake.
Kuna watu wengi sana huko duniani wanateseka sana, adui shetani anawatumikisha katika dhambi, wameshindwa kutoka kwa sababu hata watu wa kuweza kuwatoa hawapo. Ndiyo maana akasema watenda kazi ni wachache. Lakini mimi na wewe tunao uwezo wa kuifanya kazi ya BWANA ya kuvuna endapo tutaamua kujitoa kwa dhati kama wale Mitume walivyoweza kujitoa.
Asanteni sana.

No comments:

 

Top

Back To Top
 
Blogger Templates